30 Okt 2013

HII NDIO ADHABU WALIOPEWA WANAJESHI WALIO IBA VITU WESTGATE WAKATI WANAPAMBANA NA MAGAIDI.

Wanajeshi wawili nchini Kenya wamefutwa kazi na kufungwa jela kwa kitendo cha kupora mali wakati wa shambulizi la kigaidi kwenye Jengo la Westgate mwezi jana.  Hayo yamesemwa na mkuu wa jeshi la Kenya, Julius Karangi.


Karangi amesema kuwa mwanajeshi wa tatu aliyeshukiwa kwa uporaji anachunguzwa.

Awali Karangi alikanusha kuwa wanajeshi walifanya uporaji kwenye jengo hilo licha ya picha za CCT kuonyesha wanajeshi wakibeba mifuko ya plastiki kutoka kwenye moja ya maduka makubwa yaliyokuwa ndani ya Jengo la Westgate.

Hivi karibuni wanamgambo wa Somalia, al-Shabaab walikiri kufanya shambulizi hilo na kuwateka  nyara Wakenya kadhaa waliokuwa ndani ya jengo hilo kwa siku nne.

Watu 67 walifariki na mamia ya wengine kujeruhiwa.

Wakati huohuo, mkuu wa kitengo cha uchunguzi wa uhalifu katika idara ya polisi,Ndegwa Muhoro alisema kuwa mmoja wa magaidi waliokuwa ndani ya jengo hilo walipiga simu nchini Norway wakati walipovamia jengo hilo.

Mmoja wa washukiwa wa shambulizi hilo ametajwa kuwa Hassan Abdi Dhuhulow mzaliwa wa Somalia ambaye ana uraia wa Norway.

Jeshi limesema kuwa magaidi wote wanne waliofanya shambulizi hilo waliuawa.